WAGUMU ni binadamu, uongozi ni rahisi,
Na wakiwa na elimu, wepesi kwenye maasi,
Wale wasiofahamu, nao ni kama farasi,
Menejimenti rahisi, wagumu binadamu.
Kulea utaalamu, ni maongozi halisi,
Mwenyewe kujifahamu, hii ni kubwa sayansi,
Atajua majukumu, kwa wenzake kina nasi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Watu wakikutuhumu, kuwaongoza yabisi,
Wakikuona dhalimu, amri zako nakisi,
Na kama sio mwalimu, wanafunzi hukuasi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Silaha sio kalamu, ila kujaza nafasi,
Kwao kilicho muhimu, taliki ubinafsi,
Ukiwa mtu rahimu, hukwepuka nuksi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Kazi hii si kukaimu, yataka kutanafasi,
Kuyabeba majukumu, mbele yake ikhlasi,
Kunusuru wanadamu, budi kutokwa kamasi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Uongozi uimamu, haukubali maasi,
Kujua hili muhimu,kikamilifu si kipisi,
Kulimbikiza dawamu,ni laana na mkosi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Mipango budi idumu, wajibu wataka kasi,
Uratibu ni adhimu, nao hupima kiasi,
Uongozi ni jukumu, kwa njia kuziakisi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Daawa mustakimu, na isiyo na najisi,
Nasi haitugharimu, wala haina uyabisi,
Humfaa mhashamu, baraka kuwa fususi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Maamuzi ni muhimu, yakisukwa kiususi,
Yakalenga kinajimu,vitendo vyenye hamasi,
Kustawi wanadamu,bila mola kumuasi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Udhibiti si haramu, watu kukosa wepesi,
Twataka kutakadamu, na si nyuma kudurusi,
Wawekezaji adimu, wenye kuvaa libasi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
Tumtangulize rahimu, ni wetu Afu Qudusi,
Katuumba binadamu, bali sisi twamuasi,
Ukhalifa tunakimu, watokeze wafuasi,
Menejimenti rahisi, wagumu ni binadamu!
No comments:
Post a Comment