Klabu hakuna nchini, kilichopo ni utani,
Nijiunge timu gani, ushindi inayothamini,
Sio wa hapa nchini, bali kote duniani,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Haijastawi fani, hakika hapa nchini,
Mechi zetu zote duni, ya kuangalia sioni,
NInashindwa kiwanjani, kwenda kukaa juani,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Ukianzia golini, golikipa siwaoni,
Hawatoi tumaini, wakienda ugenini,
Njaa imewazaini, kukimbilia golini,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Mabeki kama katuni, sijui alowasaini,
Mpira waenda golini, wao hawalibaini,
Kufungwa kwao amini, hawawi masikitikoni,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Mawinga siwaoni, wajuao kimiani,
Wala hawana kanuni, na mfumo siubaini,
Wanitia mashakani, kufungwa hata nyumbani,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Mafowadi masikini, hawapo hapa nchini,
Wanatoka ugenini, hili jamani kwanini?
Nakiona kisirani, na balaa baluwani,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Makocha twawathamini, watokao ughaibuni,
Kazi yao siuoni, ila ujira makini,
Shahata kumbaini, bado hili ndotoni,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
Tumgeukie Manani, michezoni tushaini,
Dua haiyamkini, ziilete afueni,
Tujulikane barani, kama sio duniani,
Sijiungi na klabu, isoshinda kimataifa.
No comments:
Post a Comment