KAMA mnavyotambua, upacha yetu tabia,
Mme na mke twajua, ni wawii kijinsia,
Na kushoto na kulia, ni pande mbili za njia,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Wabunge wanapojaa, bungeni kwenda kukaa,
Wote wa chama ikawa, basi jua hapo jaa,
Rahisi kurubuniwa, patupu ukaambulia,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
'Ndio' wataitikia, hata kama ni kukuua,
Ili mradi wapewa, posho zenye manufaa,
Haliyo hawatoijua, wala kuizingatia,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Vijijini mwaumia, chama mosi kuwaoa,
Vichwa vimewajaa, wenyeviti wasojua,
Kijiji kinadumaa, ni vigumu kuendelea,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Wanasiasa balaa, sikuzote huwahadaa,
Watoto huwadhania, hamtawashtukia,
Pipi mtazingojea, mwaishia kuzisikia,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Vyema ndoa kukataa, waume wawili wakawa,
Mkeo kimoja ikiwa, wewe cha pili kuingia,
Yanga na Simba kuwa, wallahi mtaendelea,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Kama nyote Yanga mwawa, nyumba itasinzia,
Au simba tu mkawa, huzubaa familia,
Msisimko hujaa, vyama vingi kuingia,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Chagua kuendelea, ukiritmba kataa,
Chama kimoja balaa, hakiwezi kukutetea,
Wao wenyewe hung'aa,wewe ukawa wafubaa,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
Ushindani maridhia, ndivyo unavyotakiwa,
Pande mbili kuvutia, kule mtu alikokaa,
Na nchi inaposogea, hatuwapi wasiofaa,
Ndoa na chama kimoja, hukufikisha pabaya.
No comments:
Post a Comment