Ulisikiza umbeya, kisha ukauamini,
Ukweli hukuchungua, uamuzi kusaini,
Laiti ungelijua, ungefanya tathmini,
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
Wito wako nakataa, kwa sasa sikuthamini,
Cheo nimeshakuvua, ni kuruta wa kambini,
Abautani rejea, hutonikuta uani,
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
Nyikani hujatembea, utajua ya jangwani?
Ukweli hukuzoea, hakika utabaini?
Haki unaichezea, pepo ipi utawini?
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
Maiti nawatambua, wote waso nithamini,
Hata hai wangekuwa, kwangu hawana thamani,
Maisha hujiendea, Hai nikimtumaini,
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
Yakini sikuzaliwa, kuwa mchache wa imani,
Ila kumtumikia mtu hilo siamini,
Ni Muumba ya Alaa, mtumwa namuamini,
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
Ndiye wakunichagua, kwa anayoyabaini,
Mikono huitumia, kufanya yake yamini,
Na akili huteua, akanipa umakini,
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
Moyo huutangulia, pasiwe na uzaini,
Nalo analoamua, kumtii nathamini,
Kiumbe njia najua, sifuati ya shetani,
Ulisikiza umbeya, wito wako nakataa!
No comments:
Post a Comment