Na twalikitatizika, kunako siku za nyuma,
Na wengine kuudhika, kurasa mlipotunyima,
Kwaisha kunung'unika, mmetuona adhama,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Gazeti linasifika, kot Afrika nzima,
Sanaa yahitajika, kwalo msirudi nyuma,
Ushairi kwa hakika, hufanza kitu kizima,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Gwiji wanayoandika, yanayo kubwa kalima,
Wananchi hujaongoka,wakazijua azma,
Na maisha huboreka, kujengeka nchi nzima,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Ushairi kuushika, ni kitu cha lazima,
Mbali nyie mtafika, wengine warudi nyuma,
Gazeti litauzika, mzijaze ndarahima,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Mtaamsha Afrika, Kiswahili kuwa chema,
Lugha ikajapanuka, kwenea dunia nzima,
Nakala zikauzika,hata Afrika nzima,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Waulize wenye rika, waandishi waadhama,
Mapinduzi kuja zuka, mchango walitwazima,
Kuwaenzi kina kaka,ushairi kuupema,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Kuasa wataasika, viranja na maamuma,
Nchi kutoterereka, tukawa taifa zima,
Hao wanaobweteka, kuwaamsha lazima,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Ili lugha kutumika, katika dunia nzima,
Mwananchi ni mshirika, kwa manufaa ya umma,
Nadhiri budi kuweka, lugha ngeni kututuma
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Kizungu tulikitaka, watoto wende kusoma,
Mambo yamebadilika, Uchina nako lazima,
India inatwalika, Aghakan keshasema,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
Sisi tumefurahika, twawaombea uzima,
Mhariri mshirika, na wasanifu ulama,
Mashairi mtachoka, kwenu tutakavyoyatuma,
Mwananchi sasa hongera, kuuenzi ushairi!
No comments:
Post a Comment