Wengine kutumikia, binadamu ameumbwa,
Hili ni kama sheria, haustahili kuombwa,
Kutuma na kutumiwa,kila mwomba huombwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
Hautoifurahia, dunia usiyoombwa,
Pengine utashangaa, kitu gani umekumbwa,
Au utajidhania, ilviyo haukuuumbwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
Porini ukibakia, na tufani umesombwa,
Wanyama hukwangalia, kama vile hujaumbwa,
Hawatakusogelea, bila ibra kuwambwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
Au jangwani kwingia, na mchanga umesombwa,
Peke kiumbe ukawa, kwa hari utalambwa,
Upweke hukuzidia, ukajutia kuumbwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
Jela walioingia, kwa kosa moja kubambwa,
Kuta zikawazuia, kujipamba na kupambwa,
Huwehuka wakalia, wafungwa wanavyochambwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
Ndani ukijifungia, hata vipi kumerembwa,
Utumwa utajisikia, hadimu haujasombwa,
Uhuru ukalilia, nje uende kuwambwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
Raha ni kutumikia, na sio bure kubebwa,
Fani hiyo yawafaa, wanaopenda kulambwa,
Yule anayejisikia, katu hawezi kufumbwa,
Binadamu ameumbwa,wengine kutumikia.
No comments:
Post a Comment