Udikteta ndoto mbaya, mjinga akija kuwa,
Akiongoza huumia,wajinga na wanaojua,
Ni watu wa kupepewa, na moto kukokewa,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Na huyu mtu akiwa, mwenyewe tu huamua,
Zimbabwe angalia, sasa kinachotokea,
Na Malawi kaingia, mtu tusiyemdhania,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Gaddafy haukujua, yaliyomfika Libya?
Mubarak anajuria, Misri aliyoyazua,
Na Kenya hukuijua, Moi alipsimamia?
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Museveni naye pia, haya hatukumdhania,
Uganda kaikomboa, na sasa anaibomoa,
UKubwa una hatia, kwa watu wasiosikia,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Muumba namshangaa, watu hawa kuvumilia,
Sijui anadhania, watakaa kujutia,
Akawapa msamaha, mauti hajawajia,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Hujifanya wanajua, hata wasiyoyajua,
Wengine huwadhania, mabaya kuwafanzia,
Kwao si kazi kuua, ukubwa kuutetea,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Shirika nalo balaa, dikteta huliua,
Ukititimba huzaa, maradhi yasiyotibiwa,
Hadi huja kusinyaa, lenyewe likajifia,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
TTCL angalia, ugonjwa hatujajua,
Ukimwi utadhania, wala hautaelewa,
Mbona wengine wang'aa, lenyewe lazidi fubaa?
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
TANESCO ni baa, giza na bei kupaa,
Hakuna asiyejutia, 'ovataimu' kuliua,
Wingi wa watu kujaa, na kazi zinazubaa,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
TRC ng'amua, na TAZARA inayosinyaa,
Ukiritimba waviua, ushindani unapwaya,
Mameneja wenye njaa, ni shamba la kujivunia,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Ukiritimba tabia, wananchi isyofaa,
Na hii ya chama ikiwa, wanachama huenguliwa,
Mamluki wakajaa, mifuko yao kujaa,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Na ujinga nahofia, hili unalisaidia,
Wafuasi wakijua, uongozi hupindua,
Udhaifu kukataa, na wengine kuchagua,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Chama kibaka kikiwa, nchi kuisanzulia,
Wananchi huwa wakiwa, wasijue pakukimbilia,
Nusura haitatokea, bila sauti kutoa,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
Ni sauti ya kukataa, kwa hapo tulipofikia,
Mapinduzi kuyazua, watu wapya kwingia,
Afueni kuitwaa, nchi ipate endelea,
Ukiritimba mbaya, huongozwa na wajinga!
No comments:
Post a Comment