Uchumi kuwa huria, twataka viranja wapya,
Fani wanaozingatia, na ustadi kujaliwa,
Wajifanyao wajua, hatutaki wasikia,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Nchi hii ni dunia, mipaka imesambaa,
Tunatakiwa mikoa, yote kujitegemea,
Huru ikaachiwa, uchumi kuunyanyua,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Asiwe wa kuteua, mkuu wetu wa mkoa,
Twataka kumchagua, kiongozi anayefaa,
Uchumi kuuinua, mkoa wetu ukapaa,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Awajibike jamaa, kwa wakazi wa mkoa,
Kama inavyoendelea, Ujerumani Ulaya,
Nchi imejigawa, huru mikoa ikawa,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Uwekezaji wakua, viwanda vyashindaniwa,
Uzalishaji wakua, na masoko yazagaa,
Hadi sasa wasaidia, homa waliozidiwa,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Magari washadidia, BMW mwazijua,
Mercedes Benz radhia, ndiko zinakotokea,
HIi mali ya mkoa, kwa nchi inachangia,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Kilimo wamekomaa, walima kiteknolojia,
KIla mkoa wazaa, cha kula na kujiuzia,
Mayuro wajivunia, na nchi inaendelea,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Biashara waingia, kimataifa wapaa,
China wanakouzia, vyombo vyaaminiwa,
Mjerumani kifaa, nani asiyemjua,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Ni mikoa kutumia, soko, viwanda kua,
Raia kugombania, wao vya kwao bora kua,
Ni heshima na ushujaa, zikiwa bora bidhaa,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Elimu wanaojua, watoto kutufundushia,
Mitaala kuchagua, nchi inayoiifaa,
Na masomo kupungua, si ya kikapu kujaa,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Huduma wlaiobobea, wafaa wao kutoa,
Pasiwe wa kulegea, kazi akakabidhiwa,
Nchi kuendelea, imara tunatakiwa,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Wazee watasogea, pembeni wakasinzia,
KIla wakishtuliwa, mambo wataangalia,
Nchi itasisimua, na wengine kuvutia,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Vijana kuangalia, wapi tuanelekea,
Nasi bila kubagua, nafasi kuwamwagia,
Na wale wanaojua, kutufikisha hatua,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
Hakuna kupendelea, hata kwa tuliowazaa,
Kama wasipojua, vingine kuwasaidia,
Ila kama wanajua, wastahili kwendelea,
Uhuru wa kiuchumi, wataka vinara wapya!
No comments:
Post a Comment